SIMBA SC itaondoka Dar es Salaam mapema Alhamisi kwenda Songea mkoani Ruvuma kwa ajili ya mchezo wa Ligi Kuu ya Vodacom Tanzania Bara dhidi ya wenyeji Maji Maji.
Wekundu hao wa Msimbazi wataondoka baada ya mchezo wa kirafiki dhidi ya Mamelodi Sundowns Jumatano Uwanja wa Taifa, Dar es Salaam.
Mkuu wa Idara ya Habari na Mawasiliano ya Simba SC, Hajji Sunday Manara alisema jana kwamba watautumia mchezo dhidi ya Mamelodi kama sehemu ya maandalizi ya mchezo wao na Maji Maji.
Simba SC itaingia kwenye mchezo wa kirafiki na Maji Maji ikitoka kufungwa 1-0 na Azam FC Jumamosi katika Ligi Kuu.
Kipigo hicho kiliipunguza kasi Simba SC katika mbio za ubingwa na kujikuta wakiwapisha kileleni mabingwa watetezi, Yanga ambao juzi walishinda 2-0 dhidi ya Mwadui FC ya Shinyanga.
Sasa Simba ili kurudi kileleni watatakiwa kushinda dhidi ya Maji Maji Jumamosi mjini Songea, huku pia wakiiombea dua mbaya, Yanga ikwame kwa Stand United Jumapili.
No comments:
Post a Comment